Mkuu wa Wilaya ya Morogoro Regina Chonjo ameuagiza uongozi wa Manispaa kupitia upya gharama za ujenzi wa stendi ya daladala ambazo ni shilingi bilioni 5.2 ili kujiridhisha kama fedha hiyo inaendana na ukubwa wa mradi.
Mkuu huyo wa Wilaya ameyasema hayo Oktoba 29 mara baada ya kufanya ziara ya kukagua mradi huo na kutoa agizo hilo ambapo pamoja na kutoridhishwa na kasi ya Mkandarasi ametilia shaka gharama ya ujenzi zilizobainishwa kutokana na aina ya majengo yanayojengwa katika eneo hilo la stendi.
Akitoa taarifa mbele ya DC,Mtaalamu mshauri wa mradi Antonio Mpinga kutoka kampuni ya Howard Humphrey ameeleza ujenzi wa stendi hiyo utagharimu kiasi cha Bilioni 5.2 ambapo jengo la utawala litagharimu zaidi ya mil 400,Jengo la vyoo Tsh Mil 256,stoo Tsh Mil 40.
DC Chonjo ameeleza kusikitishwa na ukubwa wa gharama hizo na kueleza kuwa tukumbuke kuwa fedha hizo ni za mkopo na zitatakiwa kurejeshwa hivyo tuwe wazalendo kwa nchi yetu na wakandarasi wawe wanaandika bei zinazoendana na ukweli na amewaagiza TAKUKURU kukagua mikataba iliyopo na kujiridhisha na matumizi ya fedha.
Aidha Chonjo amemwagiza mkurugenzi wa Manispaa kuangalia upya mikataba hiyo na kuhakikisha inaendana na hali halisi,pia amemwagiza mkandarasi anajenga kuhakikisha mradi huo unakamilika kabla ya tarehe 31 Desemba.
Akiwa katika ziara ya kukagua miradi,Dc Chonjo pia amekagua miradi mingine miwili ya elimu katika shule ya msingi Azimio na sekondari ya Kingolwira ambazo zimepata fedha za fidia kutoka SGR baada ya maeneo ya shule hizo kuchukuliwa kwaajili ya ujenzi wa reli ya kisasa na kueleza kuridhishwa na kazi zilizofanyika kwa kutumia fedha hizo.
Baada ya ukaguzi Chonjo ameuagiza uongozi wa shule ya sekondari kingolwira kuhakikisha wanaanza ujenzi wa uwanja wa michezo kwaajili ya wanafunzi na kusisitiza kuwa serikali inatoa fedha ili kuona matokeo mazuri ya kazi.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro
Anuani: 166 morogoro
Simu: 0232614727
Simu: 0734-039300
Baruapepe : info@morogoromc.go.tz
Hatimiliki ©2017 Halmashauri ya Manisaa ya Morogoro. Haki zote zimehifadhiwa